Saturday, April 20, 2013

Obama asifu watu wa Boston kwa uvumilivu

 20 Aprili, 2013 - Saa 09:57 GMT

Baada ya polisi kufanya msako mkubwa mjini Boston, Marekani, wamemkamata mtu wa pili anayeshukiwa kushambulia marathon ya Boston kwa bomu.
Polisi wa Boston wanapeana hongera kwa kumpata mshukiwa wa pili
Kijana huyo alikutikana amejificha kwenye mashua baada ya mtu mmoja aliyeona mchirizi wa damu kuwazindua polisi.
Mshukiwa huyo mwenye umri wa miaka 19, na anayetoka katika eneo karibu na Chechenya, Urusi, Dzhokhar Tsarnaev, alikamatwa baada ya kufyatuliana risasi na polisi.
Amejeruhiwa vibaya na anatibiwa hospitali.
Wakaazi wa mtaa huo walipiga makofi na kushangilia wakati anaondoshwa na polisi kwa gari.
Rais Obama aliwasifu polisi na watu wa Boston kwa uvumilivu wao wakati wote wa shambulio na msako.
Piya alisema ni wazi kuwa washambuliaji wameshindwa.
Alisema watu wanataka kujua kwanini shambulio hilo limetokea:
"Bila ya shaka kuna maswala mengi hayakujibiwa.
Moja ni kwamba kwanini vijana waliokulia na kusoma hapa, wakiwa sehemu ya jamii yetu na nchi yetu, wanafanya kitendo cha maafa kama hiki?
Walipanga vipi na kutekeleza mashambulio hayo?
Na jee walisaidiwa?
Familia za wale waliouliwa kiholela wanastahiki kupata jawabu.
Majeruhi ambao baadhi yao sasa inabidi wajifunze kusimama, kutembea na kuishi tena wanahitaji jawabu.
Kwa hivo nimeliambia shirika la upelelezi la FBI na Idara ya Usalama wa Taifa na maafisa wa ujasusi kuendelea kutumia njia zote kuendeleza uchunguzi na kulinda wananchi wetu."

No comments:

Post a Comment