Monday, December 31, 2012

Chadema: Katiba Mpya si kwa ajili ya uchaguzi

kabwe


 
 
 
 
 
 
Rate This

Chama  cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimewataka wanasiasa kuondokana na fikra kwamba, Katiba Mpya ni kwa ajili ya uchaguzi tu badala yake watambue kuwa ni kuweka mpango wa namna gani Watanzania wameamua kujitawala.
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe, alisema hayo jana wakati wa mjadala wa kutathmini hali ya ya siasa Tanzania mwaka 2012 uliorushwa na kituo cha televisheni cha Startv.
Mbali na Zitto, viongozi wengine walioshiriki mjadala huo, ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Mwigulu Nchemba, na Naibu Katibu Mkuu Chama cha Wananchi (CUF), Julius Mtatiro.
“Katiba mpya siyo kwa ajili ya uchaguzi. Katiba isiwe njia ya kuwaweka madarakani wanasiasa. Tuipe ushirikiano Tume ya Mabadiliko ya Katiba iweze kufanya kazi zake vyema,” alisema Zitto.
Alisema mwaka 2013 ni muhimu sana kwa sababu vyama vya siasa na taasisi nyingine vitapeleka mapendekezo yao jinsi katiba mpya inavyotakiwa kuwa kwa Tume hiyo.
Akichangia mjadala huo, Mtatiro alisema chama chake kitaendelea kupigia debe suala la kuwapo na serikali tatu.
Mtatiro alisema katika suala la Muungano wa mkataba, CUF itatoa tathmini mwaka 2013.
Akizungumzia elimu, alisema Watanzania wanaishi katika nchi moja, lakini bado kuna ubaguzi katika hilo kutokana na shule za kata, ambazo CCM wanatamba kuzijenga, kusoma watoto wa walalahoi pekee.
“Tunakubali shule zimejengwa. Lakini mbona wanasoma watoto wa maskini tu katika shule hizi za kata? Hakuna hata mtoto wa kigogo anayesoma katika shule hizo,” alisema Mtatiro.
Naye Nchemba alisema serikali itayafanyia kazi madai ya wananchi wa Mkoa wa Mtwara waliyoyatoa kupitia maandamano waliyoyafanya Desemba 27, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment