Monday, June 3, 2013

Waingereza pia wana “Kero za Muungano”

Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron akihutubia katika mkutano wa EU mwezi Mei 2012 huko Ubelgiji
Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron akihutubia katika mkutano wa EU mwezi Mei 2012 huko Ubelgiji
Licha ya kupita miaka 40 tangu Uingereza ijiunge na Muungano wa Ulaya ( wakati huo jina lilikuwa Jumuiya ya Uchumi ya Ulaya), bado mabishano yangaliko miongoni mwa raia wa visiwa hivyo kuhusu „kero“ ndani ya Muungano huo, na kama ni bora hivi sasa nchi hiyo ijitoe. Hali hiyo imezifanya nchi nyingine shirika ndani ya Muungano huo kulalamika kwamba Uingereza ni korofi, inazuwia mwenendo wa kuzidi kuiunganisha Ulaya itakayokuwa imara zaidi na huenda siku moja kuwa na serikali moja.
Licha ya kwamba Januari mwaka huu waziri mkuu wa Uingereza, David Cameron, alitangaza kwamba huenda, baada ya uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2015, na pindi yeye atashinda katika uchaguzi huo, Waingereza wakatakiwa wapige kura ya maoni hapo mwaka 2017 kama wanataka nchi yao ibakie ndani ya Muungano wa Ulaya, bado kuna wabunge kutoka chama chake mwenyewe cha Conservative walioonesha hawajatosheka tu na ahadi hiyo ya kiongozi wao. Walitaka zaidi, na kumbinya Cameron aweke wazi- kupitia sheria itakayotungwa- kwamba kura hiyo ya maoni hakika itafanyika, na isitegmee chama chake kushinda uchaguzi ujao au yeye kubakia madarakani hadi wakati huo. Pia wala isitegemee matokeo ya mashauriano ambayo Uingereza inataka yafanyike ili ijipatie masharti mepya yalio bora kuweza kubakia katika Muungano huo.
Wiki iliopita wabunge 130, wengi wao wakiwa kutoka Chama cha Conservative ambao wanakerwa na mfumo wa Muungano wa Ulaya na namna nchi yao inavotendwa, waliwasilisha bungeni mswada uliolaumu msimamo wa serikali yao kuelekea Muungano huo. Ilikuwa kama kumpiga kibao cha usoni David Cameron. Mswada huo ulishindwa kupita bungeni, lakini ulitoa ishara muhimu ya kisiasa.
Ni wazi kwamba hisia za Waingereza wengi kupinga nchi yao kubakia ndani ya Muungano wa Ulaya  zinazidi, japokuwa wachache kati yao ni kutokana na uzalendo kuliko kuangalia hali halisi ya mambo. Mada juu ya werevu wa kuitisha kura ya maoni inabakia katika vichwa vya habari, na hata katika chaguzi za karibuni za serikali za mitaa chama cha Ukip, kinachotaka Uingereza itoke kutoka Muungano wa Ulaya, kilifanikiwa kupata kura nyingi za kutoka wanachama wa chama tawala cha Conservative. Chama hicho cha Ukip katika uchaguzi ujao huenda kikaweza kukipotezea ushindi chama cha Conservative, na kuwacha njia wazi kwa chama cha Labour kuingia madarakani. Wanachama wengi wa Chama cha Conservative hivi sasa wanataka viongozi wao watamke wazi na bayana kuhusu nchi yao kubakia ndani ya Muungano.
Kilichowaudhi wabunge hao waliowasilisha mswada wao ni kwamba katika hotuba ya karibuni alioitoa malkia bungeni- ambayo ni programu ya serikali kwa siku zijazo- hakujatajwa kwamba serikali itawasilisha rasimu ya sheria bungeni kuhusu kuitishwa kura ya maoni. Kwa hakika David Cameron asingepinga serikali yake kuwasilisha rasimu ya aina hiyo. Lakini ana tatizo. Nalo ni kwamba serikali yake ni ya mseto ambapo ndani yake kuna chama cha Liberal Democratic kinachopinga au mara nyingine kutia na kutoa kuhusu suala la kuitishwa kura ya maoni. Kwa hivyo, Cameron alijitafutia njia ya katikati, kuihifadhi nafasi na heshima yake ya kisiasa katika chama chake na, wakati huo, angalau, kuwaridhisha wabunge wa chama chake. Aliwakubalia kichinichini wabunge hao wawasilishe mswada wao, akijuwa wazi kwamba hautapita, kwani utapingwa na kura nyingi za wabunge wengine wa chama chake cha  Conservative, wale wa chama kikuu cha upinzani cha Labour na pia wa chama cha Liberal Democratic. Na hilo ndilo lilotokea.
Kama yalivyo mabishano miongoni mwa raia, hali ni vivyohivyo ndani ya vyama vikuu vya kisiasa huko Uingereza. Chama kikuu cha upinzani cha Labour, licha ya kufurahia mabishano yaliozuka ndani ya chama cha Conservative, nacho kina wasiwasi na wazo la kuitishwa kura ya maoni, kikihofia hali itakayochomoza pindi wananchi wengi wataipa mgongo Ulaya. Chama hicho kinaiona taswira ya Uingereza itakayozidi kutengwa na Ulaya. Na japokuwa matokeo ya kura ya maoni yatabidi yaheshimiwe kwa vyovyote, lakini hakitaki kubeba dhamana wa mustakbali usiojulikana. Chama cha Labour kinapendelea Uingereza ifanye mashauriano zaidi hivi sasa na izidi kuzibinya nchi nyingine za Muungano huo ziyaridhie matakwa yake na kuziondoa zile inazoziita „kero“ za Muungano. Baadhi ya viongozi wa Chama cha Labour wameweka wazi kwamba pindi patakuweko mabadiliko ya mkataba wa sasa wa Muungano ambayo yatabadilisha wizani wa nguvu, ambapo matakwa ya Uingereza yatakubalika, basi huenda wao wataunga mkono iitishwe kura hiyo ya maoni. Na suala muhimu ni kama kura hiyo ya maoni itakuwa ni kujibu suali moja tu- nalo: Uingereza ibakie ndani ya Muungano wa Ulaya au itoke?
Waingereza kadhaa wanaziona faida za Muungano wa Ulaya kama taasisi yenye kuendeleza utandawazi na uchumi wa kiliberali ndani ya soko la watu milioni 500. Lakini wana wasiwasi juu ya mipango ya Muungano huo ya kuziwekea kanuni kali taasisi za fedha na mabenki ambayo mengi yanafanya shughuli zao mjini London, hivyo mji huo kuwa kituo muhimu cha shughuli za fedha duniani. Pia chama cha Conservative hakiridhishwi na sheria za ajira za  Muungano huo, hasa zile zinazohusu masaa ya kufanya kazi, ambazo inaona zinazibana shughuli za kibiashara za Uingereza. Malalamiko yamezagaa huko Uingereza kwamba Uingereza huwekwa pembeni yanapokuja masuala muhimu ya siasa ya fedha, kwamba Tume ya Umoja wa Ulaya huko Brussels hujititimua na kuonesha misuli kama vile ni serikali ya Ulaya, inajiingiza katika mambo ambayo ni dhamana za serikali za nchi wanachama, licha ya kuwa pia na bajeti kubwa inayopita kiasi.
Licha ya kwamba asilimia 70 ya watu wa visiwa hivyo wanataka iitishwe kura ya maoni kuhusu mustakbali wa nchi yao ndani ya Ulaya, wako baadhi yao wanaotambua kwamba kuna mambo mengi ya kuwashughulisha zaidi- madeni ya serikali yanayozidi, uchumi kukwama na kashfa za kisiasa zisizokwisha. Pia wanakumbusha kwamba nusu ya uekezaji wa moja kwa moja nchini humo unatokea nchi nyingine za Muungano wa Ulaya, na nusu ya bidhaa ambazo London inasafirisha ng’ambo zinakwenda katika nchi za Muungano. Wanadai kwamba kujitoa kutapunguza nafasi za ajira, kutafanya uhusiano wa kimataifa wa nchi yao unywee na kutapunguza utajiri wa nchi yao.
Manung’uniko hayo ya Uingereza yanawakumbusha watu wa Ulaya juu ya shakashaka alizokuwa nazo rais wa Ufaransa, marehemu Charles de Gaulle, pale Uingereza ilipoomba kuwa mwanachama wa Muungano wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Ulaya. Yeye aliashiria kwamba Waingereza, kama wanavisiwa, wana hamu kubwa ya kulinda uhuru na heshima ya utawala wao. Kinachoonekana sasa ni kwamba kwa Waingereza kwao Muungano wa Ulaya ni njia tu ya kufikia lengo walilokusudia na si kwamba Muungano huo ni makusudio na lengo lao la mwisho.
Kuna nchi ndani ya Muungano ambazo haziko tayari kuikubalia Uingereza kile inachotaka. Zinahoji kwamba nchi hiyo iliingia ndani ya klabu na ikakubaliana na mashrati ya klabu hiyo pale ilipojiunga, hivyo si haki kutaka kanuni za klabu kutoka sasa zipindwe ili kuiridhisha. Haiwezekani, na kama haitaki basi ina hiyari ya kujitoa. Na yaonesha Waingereza nao huenda wakaamua kutafuta njia mbadala.
Kwa baadhi ya wachunguzi wa mambo ni kwamba Waingereza wanautaka Muungano wa Ulaya, lakini  kwa bei wanaojiwekea wenyewe, na sio kwa bei inayokubaliwa na wanachama wengine. Waingereza wanausahau ule usemi wao wenyewe kwamba mtu hawezi kubakia na keki yake huku anaila. Pia, lakini, wananchi wana kila haki ya kutaka wapige kura ya maoni, licha ya kile kitisho cha msemo wa  Kiswahili: Mtoto akililia wembe mpe.
Othman Miraji Othman
Cologne/Ujerumani
Nambari ya simu: 0653-466577 au +49-2233-21721

e-mail:  mwinjuu@hotmail.com
Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment